Habari
Wazri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kufungua maonesho ya tano ya Viwanda vya Tanzania.
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa kesho anatarajia kuzindua maonesho ya 5 ya wazalishaji wa bidhaa za ndani ya nchi. Hayo yamesemwa leo na Naibu katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara ndugu Ludovick Nduhiye wakati akiongea na waandishi wa habari katika ukumbi wa mkutano wa Mamlaka ya Biashara Tanzania ( Tantrade) uliopo katika Wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam Katika maelezo yake amesema zaidi ya wafanyabiashara 300,zikiwemo kampuni na viwanda vya ndani vinashiriki maonesho hayo Waziri Mkuu atazindua saa nne asubuhi na kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kujionea bidhaa zinazotengenezwa ndani ya nchi. Alisema kauli mbiu ya mwaka huu inasema”Tumia Bidhaa za Tanzania, Jenga Tanzania” inayohamasisha watanzania kuunga mkono bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi. Aliongeza kuwa kwa miaka mitano sasa maonesho hayo yamekuwa yakifanyika yamechagiza maendeleo ya viwanda vya ndani ya nchi kwa kuwa washiriki wengi wamepata wasaha wa kusikilizwa na kutatuliwa changamoto mbalimbali za biashara zinazowakabili. Aidha alisema kuwa wamiliki wa viwanda, vikubwa, vya kati na vidogo wamepata wasaha wa kukutana Mawaziri na Watendaji wengine wakuu wa Taasisi zinazohusiana na masuala ya biashara kisha changamoto zao kutatuliwa. Alisema,:Hii pia ni nafasi kubwa kwa wafanyabiashara hawa wakubwa, wa kati na wadogo kukutana kujadiliana masuala mbalimbali ya biashara na wenzao pamoja na viongozi wa sekta husika, Wapo ambao changamoto zao za kibiashara zimetatuliwa huku wengine wakinufaika zaidi kwa kupata wateja mbalimbali ambao wameanzisha ushirikiano wa kikazi”. Aliongeza kuwa mbali na kuonesha biashara lakini pia maonesho hayo yanaenda sambamba na kliniki ya biashara itakayowakutanisha wafanyabiashara na wataalamu wengine mbalimbali. Naye Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania(Tantrade) Latifa Mohamed Khamis alibainisha kuwa maonesho hayo yatamalizika Desemba 9 yakiambatana na matukio mbalimbali. Alibainisha kuwa tarehe tarehe 5 kutakuwa na kongamano la wafanyabiashara ambapo litahudhuriwa na viongozi mbalimbali huku akibainisha kuwa masuala mbalimbali nyeti kuhusiana na biashara yatajadiliwa. Pia alibainisha kuwa keshokutwa kutakuwa na tamasha la maziwa ambapo kutakuwa na matembezi kuanzia Uwanja wa Taifa hadi viwanja vya sabasaba ambapo viwanda vya maziwa nchini vyote vitakuwepo kuonesha bidhaa zao. Alisema lengo ni kuwahamasisha watanzania kutumia maziwa yanayozalishwa ndani ya nchi. Pia alibainisha kuwa Septemba 7 kutakuwa na mkutano kwa njia ya mtandao ambao utahusisha mabalozi wa Tanzania wa nchi za Dubai, Kuwait, Saudi Arabia nan chi nyingine ambazo zinaendelea kuthibitisha ushiriki wao. Alisema,“najua fursa za Tanzania kuuza nje ya nchi bidhaa zake ni kubwa tena sana na wafanyabiashara wengi wamekuwa wakinufaika nazo, hivyo mkutano huo utafanyika kwa njia ya Zoom.” na kuomba watanzani kujitikeza kwa wingi katika maonesho hayo.