Kuhusu Wizara
Wizara ya Viwanda na Biashara imeundwa kwa Tamko la Serikali Na. 685 la tarehe 19 Desemba, 2025 na kupewa majukumu kupitia Tamko la Serikali Na. 686 la tarehe 19 Desemba, 2025. Katika kufikia malengo ya Dira 2050, Wizara ina nafasi ya kipekee katika kutekeleza azma ya Taifa ya kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani wa viwanda utakaozalisha ajira zenye utu kwa maendeleo ya watu na Taifa. Lengo kuu ni kuleta maendeleo jumuishi na endelevu kwa kutumia rasilimali zilizopo na hivyo kuchangia katika kuzalisha na kukuza teknolojia zinazohitajika, kutoa nafasi nyingi na endelevu za ajira katika sekta zote za uzalishajimali na kulifikisha Taifa katika kiwango cha uchumi wa Kati wa Juu (upper-middle-income) unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2050.
Wizara imeendelea kuboresha Sera na mikakati ili kuweka mazingira wezeshi ya viwanda pamoja na ufanyaji wa biashara nchini, kwa kuboresha mifumo ya uratibu na usimamizi wa utekelezaji wa Mipango, Mikakati na Programu mbalimbali za kisekta. Dhamira ikiwa ni kufikia malengo ya kiuchumi na kijamii ya maendeleo endelevu na ujenzi wa uchumi wa viwanda nchini.
Ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu yake kwa ufanisi na kufikia lengo la kuwa na Tanzania yenye uchumi imara, jumuishi na shindani wa viwanda, Wizara kwa kuzingatia mahitaji ya wakati husika, ina jukumu la kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Sera, Sheria, Mipango, Programu na Mikakati inayoweka mazingira wezeshi kwa Sekta Binafsi ili iweze:- Kujenga viwanda na kuzalisha bidhaa bora zinazokidhi mahitaji ya soko la ndani na la kimataifa; na Kufanya biashara ya ushindani katika mazingira rafiki.
Aidha, Wizara ikiwa ndiyo sekta iliyobeba dhamana ya kuratibu utekelezaji wa ajenda ya ujenzi wa uchumi wa viwanda nchini, imeendelea kujenga uwezo unaoendana na kasi ya mahitaji ya uwajibikaji katika kupanga, kutekeleza na kufuatilia mipango ya kitaifa na ya kisekta. Mipango hiyo ni pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2050 (Dira 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP IV 2026/27-2030/31), Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025, Sera mbalimbali za kisekta, Mpango Mkakati wa Wizara (2026/2027- 2030/2031) pamoja na mipango mbalimbali ya kimataifa ikiwa ni pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs). Katika kutekeleza majukumu hayo, Wizara inashirikiana na Wizara na Taasisi mbalimbali za kisekta.
