Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Viwanda na Biashara

Habari

Kamati yaipongeza CBE kwa kupanua wigo katika Mikoa 


Kamati yaipongeza CBE kwa kupanua wigo katika Mikoa 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imekipongeza Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kwa kupanua wigo wa katika Mikoa mingine ikiwemo Kampasi za  Mwanza na Mbeya.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe.Deodatus Mwanyika ( Mb) Novemba 24, 2023 wakati wa ziara ya Kamati hiyo ya kukagua utendaji na utekelezaji wa miradi ya Maendeleo inayotekelezwa na Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia CBE Kampasi ya Mwanza.

Vilevile amebainisha kuwa, kazi ya  Kamati hiyo ni kuona miradi ya maendeleo inatekelezwa  kwa wakati kama  ilivyoelekezwa kwenye bajeti ili Chuo hicho kiweze kufikia malengo yake na kuongeza idadi ya wanafunzi watakaoweza kujiajiri na kutoa ajira baada ya kumaliza masomo yao katika Chuo hicho kimkakati cha biashara.

Naye, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe Exaud Kigahe (Mb.) kwa naiba ya Waziri wa Viwanda na Biashara ameihakikishia Kamati hiyo kuwa  Taasisi zote zilizochini ya Wizara ya Viwanda na Biashara  zitaendelea kutekeleza  majukumu yake hasa katika miradi ya  maendeleo kwa wakati ili kufikia adhima ya Serikali ya Awamu ya Sita yenye lengo la kutoa elimu yenye tija kwa vijana wote itakayosaidia  kukuza sekta ya Biashara.

Aidha, ameihakikishia Kamati hiyo kutekeleza changamoto zote zilizoainishwa na Kamati hiyo  ikiwemo utengenezaji wa barabara inayotumika kwa sasa kuelekea  Kampasi ya Mwanza kwa kushirikiana na Tarura.

Awali Mkuu wa Chuo cha CBE Prof. Eda Tandi Lwoga akiwasilisha taarifa ya utendaji kwa Kamati hiyo ameeleza kuwa Kampasi ya Mwanza imepiga hatua kubwa toka kuanzishwa kwake 2007-2008 ikiwa na wanafunzi 288 na wafanyakazi 5  hadi wanafunzi  1731 na watumishi 59.

Prof. Lwoga ameeleza kuwa, mafunzo  yanayoendeshwa katika Kampasi ya Mwanza ni pamoja na:- Uhasibu, Usimamizi wa Biashara, Menejimenti ya Masoko, Ununuzi na Ugavi, Ualimu katika nyanja ya Biashara, TEHAMA, Menejimenti ya Rasilimali watu na Masoko ya Kidigitali.