Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Viwanda na Biashara

Habari

Rais Samia Azindua Kiwanda cha kuunganisha malori


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema serikali itaendelea kujenga chumi wa kisasa, fungamanishi, jumuishi na shindani katika msingi wa viwanda, huduma za kiuchumi na miundombinu wezeshi.

Aidha, Rais Samia amesema sekta ya viwanda inaongeza uzalishaji na kutoa ajira kwa wananchi, jambo ambalo ni muhim katika kukuza uchumi jumuishi na kusaidia katika mapambano ya kuondoa umasikini.

Rais Samia amesema hayo leo wakati akizindua kiwanda cha kuunganisha malori na matipa cha Saturn Corporation Limited kilichopo wilaya ya Kigamboni.

Rais Samia pia amesema serikali imepunguza kodi ya makampuni kutoka 30% hadi 10% kwa kipindi cha miaka mitano ya mwanzo ili kuchochea uwekezaji zaidi kwenye sekta ya viwanda.

Vile vile, Rais Samia amesema kiwanda hiki ni chachu ya ukuaji wa viwanda na sekta nyingine kwa kuwa kinatumia vioo vinavyozalishwa na kiwanda kingine, ambacho zaidi ya 80% ya malighafi zake pia zinapatikana hapa nchini.

Hivyo, matumizi ya bidhaa zinazozalishwa hapa chini yanapunguza gharama kwa kampuni yenyewe inayotengeneza magari na pia inaongeza manufaa ya uwepo wa kampuni hiyo kwa uchumi wa nchi.

Kiwanda hiki kitatoa ajira za moja kwa moja takribani 250 na zisizo za moja kwa moja 1,800, kuongeza mzunguko wa fedha, mapato ya serikali na kuhaulisha teknolojia.