Habari
Tanzania ipo tayari kutengeneza vifaa vya umeme yenyewe

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) amesema Tanzania ipo tayari kuzalisha bidhaa za umeme za kiwango cha juu na kuweza kuhudumia Afrika na Dunia kwa ujumla.
Dkt. Kijaji amebainisha hayo Januari 4, 2024 wakati alipofanya ziara katika Kiwanda cha Multi Cable Limited (MCL) kinachozalisha vifaa vya umeme kilichopo Keko, jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujionea vifaa vinavyozalishwa katika viwanda vya ndani na mazingira ya watumishi wanaofanyia kazi pamoja na kutatua changamoto zilizopo.
Dkt. Kijaji amesema Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha bidhaa zote zinazozalishwa zinafika katika masoko ya kikanda, Afrika Mashariki EAC, Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC na Eneo Huru la Biashara Afrika AFCFTA
na ipo tayari kuwatafutia masoko.
" Sasa ni muda wa wazalishaji wa ndani kuingia kwenye soko la Eneo Huru la Biashara Afrika kwa kuwa bidhaa wanazozalisha zinaubora na viwango vilivyothibitishwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS)" Amesema Dkt. Kijaji