Habari
Dkt. Hashil T. Abdallah afungua mkutano Mkuu wa mafundi Cherehani Mkoa wa Dodoma ( UMACHEDO).

Naibu Katibu Mkuu wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Hashil Abdallah,amesema kuwa Serikali itaendelea kuwezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo kupata mafunzo ya kuendesha shughuli zao pamoja na kuwapatia mitaji ili kutimiza azma ya serikali ya viwanda.
Dkt.Abdallah ameyasema hayo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mafundi Cherehani Dodoma (UMACHEDO) uliofanyika jijini Dodoma.
Dk. Abdallah amesema kuwa serikali ipo tayari kuwezesha wajasiriamali kufanya shughuli zao bila ya kuwepo na kikwazo chochote kwa mujibu wa sheria ili waweze kufikia malengo yao.
“Wajasiriamali wamekuwa wakilalamika kuwa moja kati ya changamoto wanazokabiliana nazo ni pamoja na elimu ya biashara pamoja na mitaji, hili sisi kama serikali tutahakikisha tunalifanyia kazi kupitia taasisi yetu ya Sido kwa kuendesha mafunzo na kutoa mitaji kwa kuzingitia vigezo”amesema Dk. Abdallah
Pia amesema kuwa pamoja na kutoa mitaji na elimu pia kupitia Sido wataendelea kuwezesha wajasiriamali nyenzo zenye ubora ili kuzalisha bidhaa zenye ubora.
“Mfuko wetu wa kuwezesha wajasiriamali unaouwezo kwa kila mtu ambaye atakidhi vigezo kukopeshwa kiasi cha Sh. milioni tano lakini pia serikali kupitia shirika la NSSF na Sido wameingia makubalinaoa na benki ya Azania ili kukopesha mtaji wajasiriamali kiasi cha Sh. milioni 50 hadi 100”amesisitiza
Hata hivyo amesema kuwa serikali inaendelea kuwasilina na mamlaka husika katika maeneo mbalimbali nchini ili kupata maeneo rasmi ambayo yatatengwa kwa ajili ya wajasiriamali kufanya kushughuli zao.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Dodoma,Mhe. Antony Mtaka amewataka wajasiriamali wa mkoa wa Dodoma, kuwa wabunifu katika shughuli zao za kila siku ili kulikamata soko la bidhaa zao.
“Msipokuwa makini ujio wa makao makuu ya serikali nyinyi manaweza kuwa waangaliaji tu na fursa zote wakachukua wageni hivyo basi mnapaswa kuvaa sura za kazi ili mfikie malengo yenu kwa kubani zaidi bidhaa”amesema Mtaka
Pia Mhe. Mtaka amewapongeza UMACHEDO kwa kuungana pamoja na kuwataka kuchangamkia fursa zilizopo Dodoma badala ya kuwa waangaliaji wa fursa zilizopo Dodoma na kuwahakikishia ushirikiano kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa kuwawekea mazingira rafiki katika utoaji wa huduma zao katika shughuli mbalimbali za kiserikali zikiwemo mbio za Mwenge.
Awali Mlezi wa umoja wa mafundi cherehani ambaye ni mbunge wa Dodoma mjini, Antony Mavunde amesema kuwa tayari jiji la Dodoma limetenga ekari 8 kwa ajili ya wajasiriamali ili waweze kukidhi mahitaji yao.
“Tumetenga kiasi hicho cha eneo lakini pia na fedha ya kuanzia kiasi cha Sh. milioni 600 kwa ajili ya kuandaa eneo hili kwa ajili ya wajasirimali katika maeneo ya Nzunguni jijini Dodoma”amesema Mavunde.