Habari
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Natu El - Maamry Mamba ameongoza ujumbe wa Tanzania katika ngazi ya Makatibu Wakuu Kisekta za Biashara, Viwanda Fedha na Uwekezaji ( SCTIFI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Natu El - Maamry Mamba ameongoza ujumbe wa Tanzania katika ngazi ya Makatibu Wakuu uliofanyika Juni 2, 2023 katika Mkutano wa 42 wa Baraza la Mawaziri wa Kisekta za Biashara, Viwanda Fedha na Uwekezaji ( SCTIFI) wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unaofanyika Mei 29 hadi juni 3, 2023 jijini Arusha.
Mkutano huo ulijadili taarifa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupokea na kujadili taarifa ya Mashauriano ya awali ya Bajeti ya Mawaziri wa Fedha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Utekelezaji wa Maamuzi ya Mkutano wa 41 wa SCTIFI, Mkutano wa Kamati ya Kisekta ya Biashara, Uwekezaji, Masuala ya Forodha, Viwango ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Taarifa ya Mamlaka ya Ushindani ya Afrika Mashariki.
Aidha, Mkutano huo unajumuisha nchi wanachama wa EAC ambao ni Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudani Kusini na DR - Congo na hufanyika kwa mujibu wa Kalenda ya Mikutano ya EAC ambapo kwa awamu hii Mikutano huo unaongozwa na Mwenyekiti kutoka wa Burundi Dkt. Faida Catherine ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Uchukuzi, Viwanda na Utalii ya Burundi.
Aidha, Ujumbe wa Tanzania umejumuisha Viongozi na Wataalamu kutoka Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na Taasisi kama Mtendaji Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) Bw. William Erio, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Dkt. Athuman Ngenya na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maeneo Maalumu ya Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje (EPZA) Bw. Charles Itembe pamoja na Maofisa wangine walioshiriki katika ngazi ya wataalamu katika Mkutano huo